************************************
NA EMMANUEL MBATILO
Shirika la Utafiti na Maendeleo la Viwanda Tanzania(TIRDO) limeendelea kutoa huduma zake katika Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa katika viwanja vya Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam ambapo wamekuja na bidhaa mbalimbali ambazo wamezifanyia utafiti kwaajili ya Maonesho na kutoa elimu juu ya bidhaa hizo.
Akizungumza katika banda la shirika hilo Mfayakazi wa TIRDO Bw.Kennan Justin amesema wameamua kuleta bidhaa mbalimbali zilizofanyiwa utafiti na shirika hilo ikiwemo teknolojia ya ngozi ambapo tunamuonesha mtu namna gani anaweza kuchakata ngozi ikawa bora kwa njia ambazo ni rafiki ambazo hazina madhara kwa binadamu na mazingira.
“Vijijini wamezoea kuhifadhi ngozi kwa kutumia chumvi na hata wengine kutokuwa na uelewa na kupeleka kukatakata ngozi zao na kuwapa mifugo au kuchimbia chini, chumvi si rafiki kwasababu chumvi ni gharama na muda mwingine chumvi huadimika lakini sisi tunakufundisha unaweza kutumia majivu kuhifadhi ngozi ambapo unayaloweka upande wa wenye nyama kwa kuiwamba vizuri ili majivu yapakae kila sehemu alafu unaiweka kwenye kivuli”. Bw.Justin.
Aidha amesema kuwa teknolojia nyingine ambayo wamekuja nayo ni pamoja na Mmea wa Mwani ambao unapatikana baharini kwenye kanda za Pwani hivyo kutokana na faida zake lukuki watu wengi wakapendelea kuanza kuulima mmea huo.
“Mmea wa Mwani ukiuchanganya na bidhaa nyingine inaleta ladha pia mmea huo unasifa nyingi ikiwemo madini joto nakadharika”. Amesema Bw.Justin.
Hata hivyo Shirika hilo lina utaratibu wa kulea watafiti mbalimbali ambapo mmoja wa watafiti alifanikiwa kugundua dawa ya korona ambayo inaitwa COVIDOL ambayo hutengenezwa kwa kutumia miti shamba.
“Dawa hii ambayo imetengenezwa na mmoja wa watafiti kutoka shirika la TIRDO imekuwa ikifanya vizuri na si kutibu korona pekee bali inatibu magonjwa mengine kama kubanwa kifua, mafua,aleji zinazosababisha mafua,homa,damu kuganda pamoja na udhoofu wa kinga mwili”. Amesema Bw.Justin