Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt.Faustine Ndugulile akizungumza mara baada kutembelea banda la Mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) kwenye Maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa katika Viwanja vya mwalimu Nyerere leo Jijini Dar es Salaam.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) Bi.Justina Mashiba akizungumza na waandishi wa habari katika banda la mfuko huo kwenye Maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa katika Viwanja vya mwalimu Nyerere leo Jijini Dar es Salaam.
********************************
Takribani asilimia 94 ya watanzania wamefikiwa na huduma ya mawasiliano huku Serikali ikiendelea kujipanga kuwafikia wengi zaidi.
Ameyasema hayo leo Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt.Faustine Ndugulile mara baada kutembelea banda la Mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) kwenye Maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa katika Viwanja vya mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Amesema sehemu zote ambazo hazina mvuto wa Biashara kupitia mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) utahakikisha unafikisha mawasiliano ili kuhakikisha watanzania kwa ujumla waweze kufurahia huduma ya mawasiliano.
“Tumetangaza zabuni katika maeneo yote ya mipakani ambayo usikivu wa mawasiliano ulikuwa unapata mawasiliano kutoka nchi jirani ili kutatua changamoto hiyo. Amesema Dkt. Ndugulile
Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) Bi.Justina Mashiba amesema mfuko huo unaendelea kutatua changamoto ya mawasiliano Vijijini ambapo kwa mwaka wa fedha 2021/22 zaidi ya shilingi bilioni 30 zimetengwa ili kupeleka huduma hiyo.
Katika hatua nyingine Bi.Justina amesema mfuko huo utahakikisha unaongeza usikivu wa redio Nchini pamoja na kugawa kompyuta katika shule mbalimbali ili kuendana na mapinduzi ya Tehama pamoja na kuwajengea uwezo vijana hao.
“Mwaka huu tumenunua kompyuta 800 kwa ajili ya shule za umma, na kila shule itapata kompyuta Tano na printer moja ili iweze kuwasaidia kwenye matatizo mbalimbali yanayohusiana na tehama” alisema Bi.Justina.