NJOMBE
Halmashauri ya wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe ambayo iliyokuwa na changamoto ya uhaba wa majengo ya ofisi za watumishi na kulazimika idara tatu tofauti kutumia ofisi moja ,hatimae imekomesha changamoto hiyo baada ya shirika la nyumba la taifa NHC kujenga na kuikabidhi jengo la kisasa lililogharimu zaidi ya bil 2.5 kati ya bil 2.7 iliyokuwa imetengwa kutekeleza mradi huo.
Halmashauri ya Wanging’ombe imekuwa na upungufu wa majengo ya ofisi za watumishi wake tangu ilipoundwa mwaka 2013 kutoka wilaya mama ya Njombe na kufanya mkoa wa Njombe ulioundwa mwaka 2012 ukimeguka kutoka Iringa kuwa na idadi ya wilaya nne na halmashauri 6.
Kwa zaidi ya miaka 3 tangu Wanging’ombe imeguka kutoka wilaya ya Njombe ,halmashauri ya wilaya ya Wanging’ombe ilikuwa imepanga katika majengo ya kanisa na kisha 2016 kufanikiwa kujenga jengo dogo ambalo nalo halikutoshereza mahitaji na kukata kiu ya changamoto ya ofisi za watalaamu jambo ambalo likaisukuma serikali kuona namna ya kutafuta fedha na kuanza ujenzi wa majengo mengine kama ambavyo katibu tawala Edward Manga na afisa mipango Emmanuel Mipango wanavyofafanua kwamba kulikuwa na tatizo kubwa la ofisi za watumishi .
“Halmashauri hii ni changa imeanzishwa mwaka 2013 hivyo inakumbwa na changamoto kubwa ya nyumba na majengo ya ofisi mbalimbali hatua ambayo ilisababisha baadhi ya idara kufanya kazi katika ofisi moja na kushusha umakini kazini,Anasema Edward Manga katibu tawala Wangingombe.
Wakiweka bayana uwezo wa jengo na sababu ya kuchelewa kwa zaidi mwaka mmoja kukamilika ujenzi wake meneja wa shirika la nyumba la Taifa NHC mikoa ya Mbeya na Njombe Ramadhan Macha na Kaimu meneja TBA mkoa wa Njombe Mhandisi mchauri Edwin Masawe wanasema kutokana ubovu wa miundombinu ya barabara na upatikanaji wa vifaa vya ujenzi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri ya Wanging’ombe Agnetha Mpangile anasema wameridhishwa na ubora wa mradi huku Abdul Kambwele ambaye ni mhandisi wa NHC akiomba kupewa miradi mingine licha ya kuchelewa kukamilika kwa mradi huo.
“Tumeridhishwa na ubora wa jengo hilo ,tunawaomba muombe kutujengea na majengo mengine kama la TRA na mahakama ya Ardhi”Anasema Agnetha Mpangile mwenyekiti wa halmashauri ya Wanging’ombe.
Ujenzi wa jengo la halmashauri ya Wanging’ombe ulianza kutekelezwa tangu mwaka 2018 na kutakiwa kukamilika 2020 jambo ambalo lilishindikana kwa sababu mabalimbali.