Afisa Dawati la Jinsia Mkoa wa kaskazini Unguja Thabit Makame Haji akifafanua jambo mbele ya wadau wa mapambano dhidi ya matendo ya udhalilishaji katika ofisi za halmashauri ya wilaya ya kaskazini B Unguja.
……………………………………………………………………………..
Na Masanja Mabula
Uwepo wa mazingira ya ushirikina kwa baadhi ya kesi za udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto ni miongoni mwa changamoto zinazikabili baadhi ya familia na wanaharakati katika mapambano dhidi ya matukio hayo katika mkoa wa kaskazini Unguja.
Kauli hio imelezwa na Afisa dawati Mkoa wa kaskazini Unguja Thabit Makame Haji wakati wa maadhimisho ya siku tatu za mafunzo yaliolenga kujengewa uwezo kwa wanajamii,viongozi wa shehia na watendaji wengine kutoka taasisi mbali mbali ambazo zinajihusisha na mapambano dhi ua matukio hayo.
Alisema ni zaidi ya mara tatu wamekua wakikutana na mazingira yanayojinasibisha wazi wazi na ushirikina licha ya kesi zao kuwa na mwelekeo mzuri ambao anaamini mtuhumiwa angetiwa hatiani na hatimae kupata adhabu ambayo ingekua fundisho kwa wengine.
Alisema kuna kesi ambayo walishughulikia tangu hatua za awali na ushahidi wote ulikamilika lakini mara baada ya kesi hio kufikishwa Mahakamani muhusika alikata kauli na kushindwa kabisa kusema lolote lile.
‘’Sisi kama dawati ilituuma sana hali hio tukahisi kabisa kuwa haki inapotea kwa matendo ya kishirikina na kweli wahusika walifanikiwa maana kesi hile iliondolewa Mahakamani na mtuhumiwa kuonekana hana hatia’’aliongezea.
Alisema kwa kuwa ushirikina umetumiwa kama mwanya kwa watendaji wa maovu hayo kuna haja sasa Serikali kupitia taasisi zake kutoondoa Mahakamani kesi za mtu alieshindwa kutoa ushahidi kutokana na imani za kishirikina badala yake kezi hizo zibakie Mahakamani hapo na kuongezwa muda zaidi.
Sambamba na hayo Afisa dawati huyo alisema anaamini yapo baadhi ya matukio ya udhalilishaji yameshindwa kuripotiwa katika kituo chochote kile cha Polisi kwenye mkoa huo kwa kuwa baadhi ya familia tayari wamekua na woga uliosababishwa na matendo ya ushirikiana.
‘’Kwa mfano sisi kama dawati tulipokea kesi kwa pale ofisini kwetu Mama Mzazi alitoa taarifa za mtoto wake kubakwa na kweli uchunguzi ulibaini kufanyika kwa kitendo cha udhalilishaji wa kingono lakini cha ajabu mama mtu alikuja kufuta kesi siku chache badae kwa kuogopa kurogwa na waliotenda tukio hilo’’aliongezea.
Baadhi ya wazazi ambao miongoni mwa watoto wao wamewahi kufanyiwa udhalilishaji walisema kuna mazingira ambayo wakati mwengine hayaridhishi na kuwafanya wakate tamaa.
Mmoja miongoni mwa mzazi ambae alishindwa kujizuia na kujikuta anaangua kilio alisema mtoto wake aliwahi kubakwa na kupewa ujauzito na kisha kujifungua mtoto njiti tangu mwaka 2017 hadi leo hii kesi yake ipo Mahakamni ya wilaya Mahonda bila kutolewa maamuzi yoyote yale jambo ambalo limemfnaya kujihisi kila myonge hana haki kwenye vyombo vya sheria.
Alisema alifika maeneo yote yaliotakiwa kufika na mtoto wake kuchukuliwa kipimo cha vinasaba (DNA) lakini kinachomsikitisha hadi leo hii hakuna hukumu yoyote iliotolewa.
Awali mtaalamu wa maswala ya afya kutoka Hospital ya Kivunge mkoa wa kaskazini Unguja Mwajuma Makame Kombo alisema mtoto yoyote yule kwa mujibu wa vipimo vyao iwapo atafanyiwa kitendo cha kuingiliwa anajuulikana na hutoa taarifa hizo haraka sana kwa wahusika.
Pia Daktari huyo alietolea ufafanuzi kuhusu vipimo vya vinasaba (DNA) mara baada ya kufanyika hukabidhiwa kwa maafisa wa jeshi la polisi ambao hujaza fomu maalumu ya kuonesha kukabidhiwa kwa vipimo hivyo na si vyenginevyo kama inavtodaiw ana baadhi ya watu kuhusika kuharibu ushahidi.
Mafunzo hayo ya siku tatu yaliolenga kutoa elimu dhidi ya udhalilishaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto yaliendeshwa na Tamwa-Zanzibar kwa kushirikiana na shirika la Action Aid Zanzibar na jumla ya watu 210 walishiriki katika mafunzo hayo yaliofanyika ofisi za halmashauri ya kaskazini B Unguja.