Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Loata Sanare (kulia) akipata maelekezo kutoka kwa msimamizi wa kituo cha kujiandikisha cha wapiga kura wakati wa kuhakiki taarifa zake kwenye uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura kwenye Kituo cha Liti Manispaa ya Morogoro.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Loata Sanare, akipigwa picha katika zoezi la kuhakiki taarifa za uboreshaji kwenye daftari la kudumu la wapiga kura.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Loata Sanare akikabidhiwa Kitambulisho chake mara baada ya kuhakiki taarifa zake.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Loata Sanare (kushoto) akizungumza jambo na Afisa Uchaguzi wa Manispaa ya Morogoro, Pendo Chagu, mara baada ya kuwasili katika Kituo alichojiandikisha.
…………………………………………………………………………………..
Na, Farida Saidy,Morogoro
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Loata Ole Sanare amewataka Wananchi wa Mkoa wa Morogoro kwenda kuhakiki majina yao katika daftari la kudumu la wapiga Kura ili kujihakikishia kushiriki kwenye Uchaguzi Mkuu ujao wa kumchagua Rais, Wabunge na Madiwani unaotarajiwa kufanyika Oktoba Mwaka huu.
Loata Sanare ametoa wito huo jana Mei 4 alipokwenda kuhakiki jina lake katika kituo cha kupigia kura cha Liti Kata ya Mlimani katika Halmashauri ya Manispaa Morogoro kituo ambacho wakati wauboreshaji wa Daftari la kudumu la kupiga kura awamu ya kwanza alijiandikisha.
“mmepata nafasi ambayo ukiitumia utamchagua kiongozi utakayemtaka, itumieni fursa hiyo, la utapata kiongozi usiye mtaka” alisema.
Hata hivyo amewataka viongozi wa zoezi hilo ndani ya Mkoa huo kutoka maofisini badala yake waende kwa wananchi kuwahamasisha kwenda kuhakiki majina yao kwenye vituo walivyojiandikisha wakati wa zoezi la awamu ya kwanza.
Naye Afisa Uchaguzi wa Manispaa ya Morogoro Pendo Chagu ameitaja changamoto iliyo jitokeza katika zoezi hilo kuwa ni kukosekana kwa picha za wananchi walio jiandikisha awali kwenye daftari la kudumu la wapiga kura huku majina yao yakionekana.
Hata hivyo, ametoawito kwa wananchi kuwa pamoja na zoezi la kuhakiki katika vituo kukamilika Mei 4 bado wananchi wanaweza kuendelea kuhakiki taarifa zao kupitia simu zao za viganjani.
Kwa mujibu Mratibu wa Uchaguzi Mkoa wa Morogoro Jacob Kayange amesema zoezi la uboreshaji wadaftari la kudumu la wapiga kura awamu ya pili katika Mkoa wa Morogoro limeanza Mei 2 na kumalizika Mei 4 mwaka huu na linaendeshwa kwa halmashauri zote tisa(9) za Mkoa huo.
Aidha, Kayange amebainisha kuwa hadi Mei 4, jumla ya wananchi waliojiandikisha upya katika daftari hilo ni 6,397, wapiga kura waliokwisha rekebisha taarifa zao ni 8,190, waliofutwa kwa kukosa sifa kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na sababu ya kufariki au sababu nyingineni 141.