*******************
Mkuu wa mkoa wa Njombe Christopher Olesendeka amekiagiza kikosi kazi kilichoundwa kufatilia madeni ya wadaiwa sugu waliosababisha kufilisika benki ya wananchi Njombe NJOCOBA kuwakamata na kuwafungulia kesi ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha wadaiwa wote ambao hajalipa madeni ya mikopo waliochukua katika benki hiyo.
Agizo hilo amelitoa mara baada ya kupokea ripoti ya kikosi kazi kilichoundwa na wajumbe wa vyombo tofauti vya usalama ambayo imeonyesha takribani mil 800,153,199 zimekusanywa ndani ya siku 41 kutoka kwa wadaiwa sugu 221 kati 336 ambao walikopa fedha kabla ya benki kuingia mufilisi.
Olesendeka kazi iliyofanywa na kikosi hicho ni kubwa kwani kitendo cha bil 1.484 kuchukuliwa na wajanja wachache kimekuwa na athari kubwa katika mzunguko wa fedha katika mkoa huo hivyo kiasi cha zaidi ya mil 600 ambazo hakijarejeshwa kitarejeshwa kwa machungu makubwa na wadaiwa.
Kuhusu deni la SACOS na AMCOS za mkoa wa Njombe Olesendeka amesema baada ya agizo alilotoa mwezi mmoja uliopita kikosi kazi kimefanikiwa kukusanya mil 342 kati ya bil 6.6 ambazo zimechukuliwa na kushindwa kurejeshwa katika vyama hivyo na kueleza kuwa hadi sasa jumla ya fedha za Ushirika na NJOCOBA bil 1.1 zimerejeshwa.
Mara baada ya kupokea ripoti hiyo ndipo mkuu huyo wa mkoa akatoa agizo kwa wakuu wa wilaya zote nne za mkoa wa Njombe kushirikiana na kikosi kazi hicho kuwabaini kokote waliko wadaiwa ili kurejesha fedha za wanyonge ili kuingia katika mzunguko ambapo zaidi ya bil 8 za ushirika na njocoba ziliondoka kwenye mzunguko.